Utangulizi
Mipaka ya maisha maana yake ni kuweka vizuizi vya kipi hakipaswi au kinapaswa kuingiliwa na watu wengine kwenye maisha binafsi
Mtu yoyote anaweza kuweka mipaka yake binafsi kutokana na sababu mbali mbali anazoona zinafaa
Ni vizuri sana kuwa na mipaka ambayo itasaidia mtu binafsi na wanao mzunguka kuishi kwa amani na heshima
Mipaka ya maisha ina faida nyingi kwa watu wa jinsia zote kwa sababu ni moja ya ishara inayotambulisha ukomavu wa akili ya mtu
Bila kusahau mipaka ya maisha huonesha kwa namna gani mtu fulani anajitambua na kujua nini anataka maishani.

Mipaka Binafsi Ya Maisha Sio Mipaka Ya Ardhi
Mipaka inayoongelewa na kumaanishwa hapa sio mipaka ile ya kuonesha ukomo wa umiliki wa ardhi za watu au nchi
Lakini pia sio mipaka inayoonekana kwa macho au kushikika kwa mkono na hisia za nje ya mwili wa mtu
Bali uwepo wa vizuizi kwenye maisha ya mtu ambavyo haviruhusu mwingine kuingilia pasi na ruhusa yake
Ile hali ya kuwa na usiri au hata uhuru wa kufurahia upande mwingine wa maisha binafsi pasi na kuingiliwa na wengine
Kwa maana kila mmoja ana haki ya kuwa na maisha nje ya kufuatiliwa au kuhitaji wengine kujua anachofanya
Na ni moja kati ya haki ya msingi ya Binaadamu yoyote yule na inapaswa kuheshimiwa na kulindwa.
Mipaka Ya Maisha Sio Ukatili Wala Roho Mbaya
Kuna ambao huchanganya kati ya roho mbaya na mipaka ya maisha ya mtu anayoweka na kutaka ifatwe
Asilimia kubwa ya watu hasa nchi za Africa na Tanzania kwa ujumla wamezoea ukarimu kupindukia
Wanaamini katika kutaka kufanya kila wanachoona ni sawa kwa watu wengine hata bila kuwaza madhara
Huona kuwa kushika au kuchukua kitu cha mtu ni haki yao kwa kisingio cha undugu au urafiki mwema
Pia huona ni sawa kutaka kuingilia maisha ya mwingine kwa nguvu za hisia zao bila kujali madhara kwa wengine
Wengi humuona yule anaeweka mipaka na sheria kwenye maisha yake kama mtu mwenye roho mbaya na dharau
Yoyote ambae ataonesha hali ya kukataa au kuchukia kuingiliwa kwenye maisha yake huonekana kiburi au jeuri
Husemwa vibaya na hata kutengwa au kuchukiwa pasi na sababu za msingi kisa kupambania haki yake mwenyewe.
Maeneo Muhimu ya Kuweka Mipaka Binafsi
- Kazini, hususani wafanyakazi wenza na maisha ya kazi kwa ujumla
- Mahusiano ya mapenzi, kati ya mume na mke au hata wachumba na wapenzi wa kawaida
- Urafiki, haijalishi aina ya urafiki iwe wa kudumu au ule wa kishkaji
- Familia, iwe ukoo mzima au ndugu wa tumbo moja
Na maeneo mengine yote ambayo yanahusisha suala zima la kukutana na watu wa aina mbali mbali kwa sababu mbali mbali
Jambo la msingi ni yoyote ambaye anahusiana kwa namna yoyote ile na mtu mwingine basi lazima kuwe na mipaka.
Aina Za Mipaka Ya Maisha
Kuna aina mbali mbali za mipaka binafsi lakini hapa tutaangalia aina zifuatazo
- Mipaka ya kihisia, kama vile kutoruhusu mwingine kuingilia hisia binafsi mfano ni kama hisia za mapenzi
- Mipaka ya muda, kuwa na muda maalumu kufanya mambo binafsi ambapo wengine hawapaswi kuutumia au kuingilia
- Mipaka ya vitu, kutoruhusu wengine kutumia vitu vyako binafsi
- Mipaka ya maongezi, kutoruhusu aina fulani ya maongezi au wengine kuvuka na kuongea mambo tofauti na makubaliano
- Mipaka ya akili na mawazo, kuwa na mawazo au maamuzi huru binafsi pasi na kuingiliwa na wengine.

Faida Za Kuwa Na Mipaka Binafsi Kwenye Maisha
- Kujenga heshima binafsi
- Huongeza hali ya kujitambua na kujua kipi mtu anataka kwenye maisha yake
- Kuepuka migogoro
- Kuweka hali ya amani na imani kwa wengine
- Kufurahia maisha kwa kiwango kikubwa
- Kurahisha ufikiaji wa malengo binafsi
- Kujenga na kuboresha mahusiano aina zote
- Kulinda thamani ya vitu vya mtu
- Kulinda afya ya akili na hisia binafsi
- Kuboresha hali ya kujitegemea kimawazo na kimaisha
- Hulinda hali ya usiri na faragha ya mtu
- Kuongeza hali ya kujiamini na uhuru wa mtu NK.
Hatua Za Kuweka Mipaka
- Jua unachotaka
Hatua ya kwanza ya kuweka mipaka ni kujua kwa undani kipi unataka kwenye maisha yako kwa dhati kabisa kutoka moyoni
- Tofautisha unachotaka una usivyotaka
Ili kujua kipi unapaswa kuwekea mipaka ni lazima kutenga yale yote usiyotaka na yale unayotaka kwa dhati na tofauti
- Andika kwenye karatasi
Mambo unayotaka,mambo usiyotaka na maelezo mafupi binafsi kwanini unahisi unapaswa kuweka mipaka hio
- Weka sheria na taratibu binafsi
Kwenye ambavyo unataka na vile ambavyo hutaki lazima uweke sheria zako na kanuni kuanzia ndani ya moyo wako kuhusu wengine
- Anza utekelezaji kwa kujulisha wengine taratibu
Mabadiliko hutaka muda hasa kama ulishazoeleka kwa namna tofauti na sheria mpya ulizoweka kwa sasa hivyo lazima kuanza taratibu kuzoesha watu wajue sheria na mipaka yako mipya
- Zoesha wengine bila kurudi nyuma
Ili kufanya wengine kutambua mipaka wasiyopaswa kuvuka kwenye maisha yako lazima kutoleta mzaha ,simama imara na usiruhu kabisa kuonekana kigeugeu au mrahisi usie na msimamo
- Onesha mabadiliko na kuchukizwa ikiwa mtu hatofuata sheria zako mpya
Usiwe mpole kupitiliza pale wengine kwa makusudi wanapovuka mipaka yako, unapaswa kuonesha kuwa huna mzaha kwenye hilo kwa vitendo ila visivyo leta madhara ya moja kwa moja
- Rudia mchakato mara kwa mara
Hakuna mabadiliko ya siku moja ila kadiri utakavyo endelea kuoesha kuwa hutanii kwenye sheria na mipaka yako ndivyo wengine huzoea na kuheshimu.
Mambo Ya Kuzingatia Wakati Wa Kuweka Mipaka Binafsi Ya Maisha
- Kutumia lugha rafiki na yenye ukarimu bila hasira wala kulazimisha
- Kuheshimu mipaka yako binafsi kwanza ili wengine waheshimu pia
- Kutoongea au kujieleza sana ila vitendo vinapaswa kuwa zaidi hasa baada ya kutoa maelezo kwa mara ya kwanza
- Kutambua na kuheshimu mipaka ya wengine kama ambavyo unataka yako iheshimiwe
- Kujua mahitaji yako kwenye maisha
- Kuonesha mabadilko kwa vitendo bila kuchekea chekea anaevuka mipaka yako
- Kutokuwa kigeugeu kwamba leo upo hivi na kesho upo vile, unapaswa kuwa na msimamo.
Hitimisho
Mipaka binafsi ni moja kati ya hatua kubwa sana ambayo huonesha kiwango cha mtu anae jitambua kwenye maisha yake
Sio wote wataelewa na kuthamini mipaka yako na wapo ambao watajenga chuki ya kudumu au hata kukupa tafsiri mbaya
Jambo la msingi ni kuzingatia kile ambacho unataka na namna unavyohitaji kuishi maisha yako
Mwisho wa siku maisha ni yako mwenyewe na wewe ndio Dereva halisi wa maisha yako na pia kila mmoja ana maisha yake .